Subscribe:

Sample text

Sample Text

Wednesday, 4 October 2017

ENDELEZO LA MAENEO NYETI MATANO YAHITAJIYO KUJIFUNZWA KIKAMILIFU ZAIDI

Kati ya yale maeneo nyeti matano ambayo yamebainishwa katika kifungu cha 79 cha ile Barua “Ut Unum Sint”, tumekwisha kulipitia lile neneo linalomhusu Mama yetu Bikira Maria, na lile linahusu mahusiano kati ya Maandiko Matakatifu na Mapokeo Matakatifu. Na katika hali hiyo, sasa tumebakiwa na maeneo matatu ambayo ni:-
(1) Eneo linalohusu Sakramenti ya Ekaristi.
(2) Eneo linalohusu Sakramenti ya Upakwa Mafuta (Ordination), na
(3) Eneo linalohusu Utawala wa Kanisa (Magisterium) ambao unakabiliwa na jukumu na mamlaka ya kufundisha na kuhifadhi Imani.
SAKRAMENTI, ISHARA WAZI
Maeneo mawili ya kwanza kati ya maeneo matatu yaliyobaki yanahusu swala la Sakramenti. Kwa kadiri ya Katekisimu yetu Sakramenti imeelezwa kuwa ni “ISHARA WAZI”.
Kwa maana hiyo, swali linalotukabili sasa ni hili: Je, jambo hili la “Ishara wazi” linaendana na Mungu wetu wa pekee wa kweli ambaye Kristo Neno la Mungu ametufumulia katika Yn.8:26 kuwa ni kweli?
Ili tuweze kuwa katika hali ya kulikabili swali hili ipasavyo, sharti kwanza tujue uhalisia wa huyu Mungu wa pekee wa kweli, na uhalisia wetu sisi watu wake.
Injili ya Kristo Neno la Mungu ambayo imetimilika katika Nyaraka za Mitume, hutuambia kwamba Mungu ni Roho (Yn.4:24) aliye Umoja wa Nafsi Tatu zisizogawanyika 1Yon.5:7 (Biblia Ndogo ya Agano Jipya) na kwamba, kutokana na hali yake hiyo, awatafuta watu wamwabuduo katika Roho na Kweli (Yn.4:23).
Hivyo, kwa kusimamia Yn.8:26 na 1Yn.5:7 Biblia ndogo ya Agano Jipya, Mungu ni “Kweli” aliye Roho katika Umoja wa Nafsi Tatu, Kweli, na Neno, na Roho Mtakatifu.
JE, MTU NI NANI?
Kuhusu mtu, Bibilia hutuambia kwamba mtu ni nafsi kwa mfano na sura yake huyu Mungu aliye Nafsi Tatu (Mw.1:26), na kwamba yeye ni wa kuhuishwa kwa Pumzi (Roho) ya Mungu na kuumbiwa mwili wa nyama kutokana na mavumbi ya ardhi kuwa maskani yake hapa duniani (Mw.2:7).
Hivyo, mtu halisi ni nafsi (utu wa ndani) anayekaa katika mwili wa nyama hapa duniani.
Kwa kushirikishwa kwake Pumzi (Roho) ya Mungu, mtu amejumuishwa katika Umoja wa Nafsi Tatu, kwamba mtu ndani ya Mungu na Mungu ndani ya mtu (1Hoh.4:13); na hivyo kuwa mshirika wa utimilifu wote wa Mungu (Efe.3:19); na hivyo, kushiriki uhalisia ule ule wa Mungu, hapa duniani (1Yoh 4:17).
Hivyo, kiuhalisia, mtu halisi au mtu wa ndani (2Kor.4:16), ni nafsi kama alivyo Muumba wake, ni wa ulimwengu wa Roho, ni wa ulimwengu wa mbinguni (Fil.3:20); yuko nje ya milango ile mitano ya fahamu za kimwili wa nyama, yaani kuona, kusikia, kuonja, kunusa na kuhisi. Hii ni milango ya fahamu katika maisha yetu ya Ulimwengu huu wa mwili wa nyama hapa duniani tunapoishi kama wageni (1Pet.1:17); na siyo katika maisha yetu ya utu halisi, nafsi katika Umoja wa Nafsi Tatu za Mungu Kweli tulikojuishwa kwa kushirikishwa Roho wa Mungu (Yoh.4:13).
Kutokana na ukweli huu, mahusiano na mawasiliano kati yetu na Mungu wetu wa kweli yanapaswa kuwa kwa jinsi alivyo Yeye aliye Roho; wala hayapaswi kuendeshwa kwa akili za kimwili wa nyama (Kol.2:18).
Hivyo, Ndivyo Mungu alivyotuumba tuenende (Efe 2:10). Shetani akaja, katutaperi, akatuua na kuharibu mpango wa Mungu kwa ajili yetu. Kristo Neno la Mungu akaja kutufanya tuwe na uzima tena (Yon 10:10). Mungu akatuhuisha tena, akatufufua na kutuketisha pamoja na Kristo Neno la Mungu katika ulimwengu wa Roho (Kol.2:13-15; Efe 2:5-6).
Hivyo, lile agizo la kututakatwende kwa Roho ni agizo linalotutaka sisi tuliokombolewa na kuokolewa twende kwa kadiri ya uhalisia wa Mungu wetu aliye Roho na anayetafuta watu wamwabudu katika Roho na Kweli kwa kuwa Yeye ni Roho (Yn.4:24).
JE, UTARATIBU WA KWENDA KIROHO UKOJE?
Katika kutufundisha kuhusu swala hili, siku moja Yesu alimwuliza Yule Ofisa, “Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa (Yn.4:48)? Tena, ona alivyomwambia Mtume Toma, “Wewe kwa kuwa umeona, umesadiki. Wa heri wale wasioona wakasadiki (Yn.20:29). Na kinyume cha “heri” ni “Ole”. Kwa kauli hiyo tunaambiwa, “Ole wao wale wanaotaka waone ndipo wasadiki”.
Katika kutimiliza Injili ya Kristo Neno la Mungu, Nyaraka za Mitume kwanza hututafsiria neno imani; kwamba ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo; ni bayana ya mambo yasiyoonekana (Ebr.11:1).
Tunaambiwa katika Ebr.11:6 kwamba pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu; maana yeye amwendeaye Mungu sharti aamini kwamba Yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao. Katika Ebr.10:38 Mungu anasema, “Mwenye haki wangu ataishi kwa imani; naye akisitasita, Roho yangu haina furaha naye”.
Katika Yak.1:6-8 tunasoma, “Ila na aombe kwa imani pasipo shaka yoyote. Maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo na kupeperushwa huku na huku. Na mtu kama huyo asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana. Mtu wa nia mbili husitasita katika njia zake zote”.
Tunaambiwa katika 2Kor.5:7; “Twaenenda kwa imani; si kwa kuona”. Na katika Gal.5:4-5 tunaambiwa, “Mmetengwa na Kristo ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria. Mmeanguka na kutoka katika hali ya neema (aliyotustahilia Mungu katika Kristo Neno la Mungu pale Msalabani). Maana sisi kwa Roho tunalizamia tumaini la haki kwa njia ya imani”.
Hivyo, sisi watu, kwa kuwa utu wetu halisi, nafsi, ni wa uhalisia wa Mungu pekee wa Kweli ulio nje ya milango ya fahamu za kimwili wa nyama, mahusiano na mawasiliano na Mungu wetu wa pekee wa kweli ni siri kati ya Mungu na mtu kwa njia ya imani; ni siri kati ya Umoja wa Nafsi Tatu na utu wa ndani, nafsi, iliyo utu halisi ihuishwayo kwa Roho wa Mungu iliyotiwa ndani ya mtu husika.
Kwa mantiki hii, ibada za kisakramenti na kivisakramenti ni ibada zilizo kinyume kabisa cha uhalisia na mapenzi ya Mungu. Tena, kwa kweli, ni ibada adui dhidi ya Mungu wa kweli anayetafuta kuabudiwa katika Roho na kweli. Hizi ni ibada za kumwabudu mungu mwingine na zinazoenendwa na yesu mwingine (2Kor.11:4). Kumwamini au kutomwamini Mungu itakiwavyo, ni swala la kibinafsi. Hakuna kufanyiana. Ndiyo maana ni siri kati ya mtu na Mungu katika kumkaribia Mungu kwa moyo wa kweli na utimilifu wa imani (Ebr.10:22). Izingatiwe kwamba neno “Imani” ni kwa kadiri ya tafsiri ya Ebr.11:1 na si vinginevyo. Si swala la kuamini yaliyotengenezwa na wakubwa fulani (Kol.2:8-10), au yale mtu anayojitengenezea mwenyewe kwa akili zake za kimwili wa nyama au nafsi yake.
ENEO LA UTAWALA WA KANISA
Eneo nyeti la tano lililobainishwa katika kifungu cha 79 cha “”Ut Unum Sint” ni lile eneo linalohusu Utawala wa Kanisa (Magisterium) ambao unakabiliwa na jukumu na mamlaka ya kufundisha na kuhifadhi imani.
Kuhusu eneo hili, hebu tuanze na Yn.6:45, Andiko ambalo hutuambia kwamba watu wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Na Yn.14:26 Yesu hutuambia kwamba Roho Mtakatifu Msaidizi atatufundisha yote na kutukumbusha yote. Tena huyo Roho wa kweli atatuongoza na kututia kwenye kweli yote, (Yn.16:13). Na 1Kor.2:10-12 hutueleza wazi kwamba Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote hata mafumbo ya Mungu. Maana ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu.
Ndiyo maana nimesema hili swala la mahusiano na mawasiliano kati ya Mungu na mtu ni siri kati ya Mungu na mtu.
Katika Mt.23:8-10 Kristo Neno la Mungu anaweka yote pamoja, “Bali ninyi msiitwe Rabi, maana Mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani, maana Baba yenu ni mmoja aliye wa mbinguni (wa uhalisia wa Roho). Wala msiitwe viongozi, maana kiongozi wenu ni mmoja naye ndiye Kristo”.
Kwamba, swala hili la mahusiano kati ya Mungu na mtu ni la kila mtu binafsi limetabiriwa na manabii. Katika Yer.31:33-34 Mungu aliahidi, “Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaandika; nami nitakuwa Mungu wao nao watu wangu. Wala hawatamfundisha mtu na jirani yake, na kila mtu na ndugu yake wakisema, Mjue Bwana; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao; hadi aliye mkubwa miongoni mwao maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena”.
Na kwa unabii wa Ezekiel Mungu alisema, “Nami nitawanyunyizia maji safi, nanyi mtakuwa safi; nitawatakaseni kutoka kwa uchafu wenu wote, na kutoka kwa vinyago vyenu vyote. Nami nitawapa ninyi moyo npya, nami nitatia roho mpya ndani yenu, nami nitatoa moyo wa jiwe uliomo ndani ya mwili wenu, nami nitawapa moyo wa nyama. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, na kuwaendesha katika sheria zangu, nanyi mtazishika hukumu zangu na kuzitenda (Eze.36:25-27).
Utabiri huu ndio ule ulioelezwa ya Yesu mwenyewe kama tulivyoona hapo juu katika Mt.23:8-10, na kutimilizwa kama ulivyoelezwa katika 1Kor.12:13; Gal.3:27 na ule upakwaji mafuta ulioelezwa katika 1Yoh.2:20, 27. Aya hizo za mwisho zatuambia, “Ninyi mmepakwa mafuta na Yeye aliye Mtakatifu nanyi mnajua nyote. Nanyi mafuta yale mliyoyapata kwake yanakaa ndani yenu, wala hamna haja ya mtu kuwafundisha; lakini kama mafuta yake yanavyowafundisha habari za mambo yote, tena ni kweli wala si uongo, na kama yalivyowafundisha, kaeni ndani yake”.
Upakwa mafuta na Roho Mtakatifu ulitabiriwa kama ahadi katika nyakati za manabii, sasa katika nyakati timilifu unaelezwa kwamba umetimilika kama tunavyohakikishiwa katika Nyaraka za Mitume zilizo utimilifu wa Injili ya Kristo Neno la Mungu.
MASWALI YA KUJIULIZA NA MAJIBU YAKE
Ndipo tunapokuwa na haki ya kujiuliza:
Je? Maeneo haya ya ishara Wazi na Utawala wa Kanisa kama yalivyo kiuhalisia, hayaendi kwa injili nyingine iliyo tofauti na ile waliyoihubiri Mitume (Gal.1:8-9) na hivyo kuenenda na injili iliyo laaniwa inayotupeleka kwa yesu mwingine na roho nyinginezo mbali na Roho wa Kweli (Kor.11-4)?
MATENDO AU MATUNDA NDIYO DIRA
Tumeamriwa na kuonywa “Wapenzi msiiamini kila roho, bali zipimeni hizo roho, kama zimetokana na Mungu, kwani kuna Roho wa kweli na roho ya upotevu (1Yon.4:1, 6).
Tena tumeagizwa, “Ufanyeni mti kuwa mzuri na matunda yake kuwa mazuri. Au ufanyeni mti kuwa mbaya na matunda yake kuwa mabaya, kwa maana kwa matunda yake mti hutambulikana. Enyi wazawa wa nyoka, mwawezaje kunena mema mkiwa wabaya? Maana kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake. Mtu mwema katika akiba njema hutoa mema; na mtu mbaya katika akiba mbaya hutoa mabaya (Mt.12:33-35) Mtawatambua kwa matendo yao (Mt.7:16, 20).
Tumeagizwa, “Basi nasema Nendeni kwa Roho, wala hatazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa maana mwili hutamani kushindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka (Gal.5:16-17).
Matendo ya kwenda kwa mwili yameorodheshwa na Paul Mtume katika Gal.5:19-21 kuwa ni: Uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, mafarakano, uzushi, husuda, ulevi, ulafi na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawambia mapema kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu wayatendao mambo ya jinsi hiyo, hawataurithi ufalme wa Mungu.
Tena twaambiwa, “Mambo hayo yanaonekana kana kwamba yana hekima katika namna ya ibada mliyojitungia wenyewe na katika kunyenyekea, na katika kuutawala mwili kwa ukali; lakini hayafai kitu kwa kuzizuia tamaa za mwili (Kol.2:23).
Twaangalishwa, “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundishao ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo. Maana katika Yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili. Na ninyi mmetimilika katika Yeye aliye kichwa cha enzi yote na mamlaka (Kol.2:8-10).
Pia, tunatakiwa tupate utajiri wote wa kufahamu kwa hakika, tupate kujua kabisa siri ya Mungu yaani Kristo; ambaye ndani yake Yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika (Kol.2:2-3).
Kiuhalisia katika maeneo haya matatu, kunakosekana kabisa jitihada za kuwasaidia wadau wa kanisa kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri ya Mungu, yaani Kristo.
Ndipo tunapoambiwa kwamba tunda la kwenda kwa Roho ni lile lilioodheshwa katika Gal.5:22-23; na katika Gal.5:4-5 twasoma, “Mmetengwa na Kristo ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria. Mmeanguka na kutoka katika hali ya neema. Lakini sisi kwa Roho twalitazamia tumaini la haki kwa njia ya Imani”.
MUHTASARI WA MAENEO MATATU YA MWISHO KATI YA YALE MATANO
Baada ya maagizo, maamuru maelekezo maangalisho tuliyoyapewa na Neno la Mungu tunahitimisha ukweli kwamba yale maeneo mawili ya kiishara wazi yako nje ya Kristo na Mungu wa pekee wa kweli anayetaka kuabudiwa katika Roho na kweli.
Na lile eneo la Utawala wa Kanisa nalo liko nje ya Kristo Neno la Mungu kwa sababu kanisa linalohusika na Utawala huu ni kanisa la kimwili na imani inayofundishwa ni ile inayosemekana katika ile sala ya Imani “Mungu wangu nasadiki ninayofunashwa kusadiki na Kanisa Katoliki la Roma; kwani ndiwe uliyefumbulia hayo. Imani hii iko nje kabisa na ile imani iliyotafsiriwa katika Ebr.11:1 na kusisitizwa katika aya nyinginezo nyingi za Biblia.
Hiki kipengele “Ndiwe uliyefundulia hayo….” Hakizingatii ukweli kwamba:-
(1) Yupo yule mwasi na mpingamizi ajiinuaye nafsi yake juu ya kila kiitwacho mungu ama cha kuabudiwa, hata yeye mwenyewe kuketi katika hekalu la Mungu akijionesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu (2Thes.2:4).
(2) Ipo roho ya upotevu (1Yon.4:6) ambayo iko kazini kuwapoteza watu wasiijue kweli wasije wakamwongokea Mungu wa kweli akawaponya (2Kor.4:3-4; Yn.12:40).
Na kutokana na dira tuliyoipewa kupimia roho, hali yakushamiri madhambi hata ndani ya wana makanisa, ni kithibiti tosha kwamba roho ya upotevu ndiyo inayoshikilia makanisa na kupofusha wana makanisa wasichomoke kutoka gereza na minyororo ya utumwa wa dhambi. Mfalme wa Uwezo wa anga, roho Yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi ndiye anayetawala, makanisa.
Hivyo, maeneo matatu yaliyotubakia yako katika uadui dhidi ya Mungu wa pekee wa kweli. Ipo haja ya kujitoa katika hali hii.
MAENEO HAYA MATATU YAKO KINYUME CHA “UT UNUM SINT”
Katika kifungu Na.1 cha Barua yake ya Kichungaji “Ut Unum Sint”, Mt. Papa Yohani Paulo II anatoa hamasa ya kupambana na mwelekeo wa dunia ya kufuta kabisa nguvu za Fumbo la Ukombozi. Katika kifungu hicho, Papa amewataka waamini Kristo kuuishi UKWELI mmoja kuhusu Msalaba, kinyume cha dunia inayokana ukweli kwamba katika Msalaba mtu ana chimbuko la uzima mpya. Dunia hudai kwamba Msalaba hauwezi kumpa mtu maono wala matumaini. Dunia husema kwamba mtu si chochote bali ni kitu cha kiudongo tu kinachopaswa kuishi kana kwamba Mungu hayupo.
Kwa kwenda kimwili wa nyama kama inavyothibitika katika maeneo haya matatu, makanisa yetu siyo tu kwamba yanaelekea, bali kiuhalisia, yanakanusha nguvu ya Fumbo la Ukombozi pale Msalabani. Kiuhalisia, makanisa yetu hayatambui Fumbo la Ukombozi ulio katika Kristo Yesu ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho kwa njia ya imani katika damu yake, ili aoneshe haki yake, kwa sababu ya kuziachilia katika ustahimili wa Mungu dhambi zote zilizotangulia kufanywa (Rumi 3:24-25). Makanisa hayatambui kwamba Mungu ametupatanisha sisi na Nafsi yake kwa Kristo pale Msalabani; yaani Mungu alikuwa ndani ya Kristo akiupatanisha ulimwengu na Nafsi yake asiwahesabie makosa yao. Kwamba Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye (2Kor.5:18-19, 21).
Kwa kutotambua ukweli huu wa wema, huruma, upendo, uwezo na namna za Mungu (Isa.55:8-13) makanisa hujitungia ibada na taratibu zao za kuhusiana na kuwasiliana na Mungu ambazo hazifai kitu kwa kuzizuia tamaa za mwili (Kol.2:23; Gal.5:19-21). Matokeo yake watu hubaki kuwa watumwa wa dhambi. Na Mungu hawasikii wenye dhambi (Yn.9:31). Ndiyo maana kuna kutengwa na Kristo, kuanguka na kutoka katika hali ya neema. Iliyobaki ni kutourithi ufalme wa Mungu (Gal.5:4-5, 21; Ebr.10:26-27, 29). Kwa kutoenenda kwa Roho, makanisa hushiriki 100% ile dhambi ya kupuuza kilichofanyika pale Msalabani.
SASA MCHAWI WETU NI NANI?
Basi niseme nini juu ya hayo? Kifupi, tumtambue mchawi wetu. Naye si mwingine, bali ni shetani. Kumtafuta mchawi mwingine nje ya Shetani ni kupoteza muda na mwelekeo. Tumeambiwa, “Hata hamwezi kufanya mnayotaka (Gal.5:17). Nafsi wewe ni nafsi tegemezi: Au kuungana na Kweli au Ibilisi. Wewe kama wewe, au mimi kama mimi, sote hatuwezi kufanya tunayotaka (Gal.5:17).
Ukihama dini au ukianzisha dini, ibilisi atakukuta huko huko. La kufanya tumekwisha kuambiwa katika 1Kor.7:20 na 24, “Basi ndugu zangu, kila mtu na “akae mbele za Mungu”, pale pale alipo. Hakikisha unakaa mbele za Mungu wa pekee wa kweli hapo hapo ulipo.
Tunaukumbuka usemi wa Papa Yohani Paulo II, Kifungu cha 80 cha “Ut Unum Sint” kwamba wote, kuanzia Maaskofu hadi waamini walei, wamepokea Upako wa Roho Mtakatifu. Tumeona matokeo ya kupokea Upako Mtakatifu ni kuingiwa na Roho Mtakatifu anayekaa ndani ya mtu kumfundisha kweli yote na kumwongoza mtu na kumtia kwenye kweli yote. La kufanya ni moja tu; nalo ni kuhakikisha unakaa mbele za Mungu wa pekee wa kweli, kwa Neno lake yaani Roho wake anayekutamani kiasi cha kuona wivu (Yak.4:5). Yeye atakunong’oneza siri yake yote (1Yon.2:20, 27). Kaa katika Neno lake (Yn.8:31-32). Hicho ndicho chakula kitiacho uzima (Yn.6: 63), tena uzima tele (Yn.10:10).
Amani yake Kristo Neno la Mungu, amani ile aliyoisema katika Yn.14:27, itamalaki ndani yako na kati yetu katika kuukulia ukweli wa Mungu kwa sifa na Utukufu wa huyu Mungu wetu wa pekee wa kweli, na kwa uzima na usalama wetu.
Na ubarikiwe kwa Baraka zote za kiroho katika ulimwengu wa roho ndani yake Kristo Neno la Mungu (Efe.1:3) sasa na hata milele.
LUKA ROKI MAGHALI CHAMAYOMBE
0787 765 759
0714 118 428
0753 298 707
Chamayombe37@gmail.com

0 comments:

Post a Comment