Subscribe:

Sample text

Sample Text

Wednesday, 4 October 2017

IMANI NI NINI, KWA NANI, KATIKA NINI NA MATOKEO NI NINI?

Katika kutafakari swala la imani, hebu tuanze na aya zifuatazo: Gal.5:16-17; Mk.10:27; 9:23 na Mt.17:20.
Gal.5:16-17 hutuambia, “Basi nendeni kwa Roho wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili, maana hizi zimepingana HATA HAMWEZI KUFANYA MNAYOTAKA.
Nafsi ya mwanadamu ambaye ni mfano na sura ya Mungu, aliye Nafsi Tatu, ilipata kuwa nafsi hai baada ya kushirikishwa uzima halisi wa Mungu mwenyewe (Mw.2:7).
Hivyo, mwanadamu kama mwanadamu ni nafsi isiyo na uhai wake mwenyewe. Na hivyo, katika hali hiyo mwanadamu kama mwanadamu hawezi kufanya kitu.
Ndiyo maana, katika Mk.10:27 Bwana Yesu Neno la Mungu, anasema “Kwa binadamu haiwezekani”, kwani hana uhai wake mwenyewe. Ndiyo maana tunaambiwa wazi, “Roho ndiyo itiayo uzima (Yn.6:63).
YOTE YAWEZEKANA KWAKE AAMINIYE [MK.9:23], WALA HALITAKUWAKO NENO LISILO WEZEKANA KWENU [MT.17:20]
Tumekwisha kupata tafsiri ya neno “IMANI” kwamba ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo; ni bayana ya mambo yasiyoonekana. Au, kwa Kiswahili kinachosemekana kwamba ni cha kisasa, “Imani ni kuwa na hakika ya mambo tunayotumainia; ni kusadiki kabisa mambo tusiyoyaona. Imani ni kuyachukulia tusiyoyaona, kwamba yamekwisha kutimilika 100%.
IMANI KATIKA NINI? AU KUAMINI NINI?
Baada ya kujua maana ya neno imani, swali linalofuata ni “KUAMINI NINI?” Vinginevyo tutabaki hewani, na hapo ibilisi atakuwa amepewa nafasi.
Katika hili, Bwana Yesu anajibu, “Mwaminini Mungu” (Mk.11:22), ambaye kwake yote yawezekana (Mk.10:27) mpate kuuvaa utimilifu wote wa uwezo wa Mungu wa kuhamisha hata milima (Mk.11:23).
KUMWAMINI KRISTO NENO LA MUNGU
Katika Yn.14:1 KRISTO NENO LA MUNGU atuambia, “Mnamwamini Mungu, niaminini na Mimi”. Kristo Neno la Mungu alikwisha kutudhihirishia kwamba Baba yake aliyemtuma ni kweli (Yn.8:26). Jambo hili lilikwisha kushuhudiwa na Yeye ashuhudiaye, Roho Mtakatifu (1 Yoh.5:7) kwamba Mungu ni kweli (Yn.3:33).
Sasa hapa atuambia, “Mnamwamini Mungu aliye kweli; niaminini na Mimi niliye Neno lake. Yn.17:17 anatusisitizia kwamba Mungu aliye kweli na Neno lake ni Umoja, pale alipomwambia Baba, “Uwatakase kwa ile kweli; Neno lako ni kweli.
MANENO YA YESU MWISHONI MWA MAISHA YAKE DUNIANI
Bwana Yesu akawaambia wanafunzi wake “Hata bado ningali ninayo mengi ya kuwaambia lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. Lakini yeye atakapokuja huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote…….” (Yn. 16:12-13)
Baada ya kufufuka kwake, pamoja na mengineyo, aliwaambia, “Amani iwe kwenu; kama Baba alivyonituma mimi, mimi nami nawatuma ninyi. Naye akiisha kusema hayo, AKAWAVUVIA, AKAWAAMBIA, POKEENI ROHO MTAKATIFU”. ( Yn.20:21-22)
Hapo ndipo utume wa mitume ulipotimilika. Maana, pamoja na kuwatuma, amewatia Roho Mtakatifu wa kuwaongoza awatie kwenye kweli yote. Na ndiyo maana Paulo ana ujasiri wa kusema “Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbiguni atawahubiria ninyi Injili yoyote isipokuwa hiyo tuliyowahubiria na alaaniwe (Gal.1:8-9). Hata anatushangaa pale tunapowavumilia wale wanaohubiri mayesu wengine na hata kupokea maroho mengine (2Kor.11:4).
Kwa nini Paulo Mtume asema haya yote? Ni kwa sababu wao walimpokea Roho Mtakatifu halisi (Original) kutoka kwa Kristo Neno la Mungu mwenyewe. Roho waliyempokea kutoka kwa Yesu asingeweza kuwa roho ya upotevu.
Wakiwa wanaongozwa na Roho wa Kweli, kwenye kweli yote wanatufundisha yafuatavyo:
(1) Basi nasema nendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili, kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana HATA HAMWEZI KUFANYA MNAYOTAKA (Gal.5:16-17).
(2) Mmetengwa na Kristo ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria; mmeanguka na kutoka katika hali ya neema. Maana sisi kwa Roho tunalitazamia tumaini la haki kwa njia ya imani (Gal.5:4-5).
(3) “….wakapate utajiri wote wa kufahamu kwa hakika wapate kujua kabisa siri ya Mungu, yaani Kristo; ambaye ndani yake Yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika (Kol.2:2-3).
(4) “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu; kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu wala si kwa jinsi ya Kristo. Maana katika Yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili. Na ninyi mmetimilika katika Yeye aliye kichwa cha kila enzi na mamlaka Kol.2:8-10.
(5) Kwa kuwa katika Yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa Yeye kuvipatanisha vitu vyote na Nafsi yake akiisha kufanya amani kwa Damu ya Msalaba wake (Kol.1:19-20a).
(6) Watu wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu; wanahesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu; ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho kwa njia ya imani katika Damu yake. apate kuonesha haki yake, kwa sababu ya kuziachilia katika ustahimilifu wa Mungu dhambi zote zilizotangulia kufanywa (Rum.3:23-25).
(7) Kristo akajitoa ili makusudi alitakase na kulisafisha Kanisa lake kwa maji katika Neno…..” Efe.5:26-27
(8) Hivyo, ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye kafara ya suluhu kwa dhambi ya watu wake (Ebr.2:17).
(9) Ndipo aliposema, “Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza kusudi alisimamishe la pili; katika mapenzi hayo, mmepata utakaso kwa kutolewa Mwili wa Yesu (Neno la Mungu) mara moja tu. (Ebr.10:7-10)
Na kila kuhani husimama kila siku akifanya ibada, na kutoa dhabihu zile zile mara nyingi ambazo haziwezi kabisa kuondoa dhambi. Lakini huyu alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele aliketi mkono wa kulia wa Mungu. Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa. Ndipo asemapo, “Dhambi zao na uasi wao sitaukumbuka tena kabisa. Basi ondoleo la hayo likiwapo, hapana toleo tena kwa ajili ya dhambi (Ebr.10:11-18).
(10) Katika Ebr.10:19-23 tunaambiwa, “Basi, Ndugu kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa Damu ya Yesu, njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia yaani Mwili wake; na kuwa na Kuhani Mkuu juu ya Nyumba ya Mungu; NA TUKARIBIE WENYE MOYO WA KWELI KWA UTIMILIFU WA IMANI HALI TUMENYUNYIZIWA MIOYO TUACHE DHAMIRI MBAYA, TUMEOSHWA MIILI KWA MAJI SAFI. NA MLISHIKE SANA UNGAMO LA TUMAINI LETU LISIGEUKE; MAANA YEYE ALIYEAHIDI NI MWAMINIFU”.
(11) Wala hawezi kujikana mwenyewe ‘ kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe”. (2Tim.2:13).
Hayo ndiyo wanayotufundisha Mitume wa Yesu Neno la Mungu kuhusu swala la ondoleo la dhambi.
YESU MWENYEWE ANASEMAJE KUHUSU ONDOLEO LA DHAMBI
Katika Mt.20:28 atuambia, “Kama vile mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa Nafsi yake iwe fidia ya wengi”. Na katika Mt.26:28 anaweka wazi zaidi: “Kwa maana hii ndiyo Damu yangu ya agano jipya imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi”.
MATOKEO YA UTAKASO AU ONDOLEO LA DHAMBI
Kwa kadiri ya Ebr.10:14, tokeo la utakaso ni kukamilishwa hata milele. Ukamilishwaji huu upo katika kushirikishwa Roho Mtakatifu (1Yoh.4:13); tendo ambalo hufanyika kwa kunyweshwa Roho mmoja (1Kor.12:13) na kumvaa Kristo Neno la Mungu (Gal.3:27); na hivyo kuwa mwana wa Mungu (Gal.3:26) kuwa kama Mungu mwenyewe alivyo (1Yoh.4:17). Na hivyo, kushiriki tabia ya Uungu (2Pet.1:4) ikiwa ni pamoja na uwezo.
Ili kufikia hilo, siri ya Mungu iko katika Yesu Neno la Mungu, nayo ni kuamini utakaso kwa Damu ya Yesu ambaye ni Roho Mtakatifu ambaye ndani yake mna maji hai (Yn.4:10, 14; 7:37-39); naye huyu Roho yumo ndani ya Neno kama vile Neno alivyo ndani ya Roho na Kweli, katika Utatu wao Mtakatifu.
HITIMISHO
Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana. Tena imani ni nguvu kuu; kwani yote yawezekana kwake aaminiye, wala hakuna Neno lisilowezekana kwake aaminiye. (Mk.9:23; Mt.17:20)
Lakini nguvu hiyo iko katika kushirikishwa utimilifu wote wa Mungu (Efe.3:19) kwa kunyweshwa Roho Mtakatifu (1Kor.12:13; 1Yoh.4:13), na hivyo kumvaa Kristo Neno la Mungu (Gal.3:27).
Ili kunyweshwa Roho Mtakatifu, kuzaliwa mara ya pili (Yn.3:3, 5), sharti mtu awe amepokea upatanisho na utakaso kwa njia ya imani katika Damu ya Yesu (Rumi.3:25; Kol.1:20; Ebr.10:19-22) iliyomo katika Neno la Mungu (Efe.5:26-27).
Nje ya hayo tunaambiwa “MAANA TUKIFANYA DHAMBI KUSUDI BAADA YA KUUPOKEA UJUZI WA ILE KWELI, HAIBAKI TENA DHABIHU KWA AJILI YA DHAMBI; BALI KUNA KUITAZAMIA HUKUMU YENYE (KWENYE) KUTISHA NA UKALI WA MOTO ULIO TAYARI KUWALA WAO WAPINGAO. MTU ALIYEIDHARAU SHERIA YA MUSA HUFA PASIPO HURUMA KWA NENO LA MASHAHIDI WAWILI AU WATATU. MWAONAJE? HAIKUMPASA ADHABU ILIYO KUBWA ZAIDI MTU YULE ALIYEMKANYAGA MWANA WA MUNGU NA KUIHESABU DAMU YA AGANO ALIYOTAKASWA KWAYO KUWA NI KITU OVYO, NA KUMFANYIA JEURI ROHO WA NEEMA? (EBR.10:26-29).
Kwa maana asema, “Kwa wakati uliokubalika nilikusikia. Na katika siku ya wokovu nilikusaidia, tazama, wakati uliokubalika ndio sasa, tazama, siku ya wokovu ndiyo sasa (2Kor.6:2).
Chakuzingatiwa kwa makini ni ukweli huu kwamba kumwamini Mungu kama Mungu hakuna thawabu yoyote. Tendo hilo hata mashetani hulifanya; tena kwa kutetemeka.( Yak.2:19).
Bali tunalotakiwa sisi ni kulitambua na kuliamini lile tendo timilifu la kutohesabiwa makosa ( Rumi.8:33-34, 2Kor.5:19) na kutakaswa kwa maji safi yaliyomo katika damu ya Kristo Neno la Mungu ambaye ni Roho Mtakatifu ( Efe 5:25-27, Ebr.10:19-22, Yoh.7:37-39)
Katika yote, siachi kumshukuru Mungu wa pekee wa kweli kwa udhihirisho wake kwenye Mtaguso wa Vatikani II na katika Mababa (Mapapa) Mtakatifu waliofuata katika utayari wao kutekeleza kusudio lake la kuumba upya dunia yake inayoharibiwa na Yule mwovu.
Kwa namna ya pekee nazingatia zile kauli za ule Waraka wa Kichungaji “UT UNUM SINT” ulioandikwa na Mt. Papa Yohani Paulo II ambao kwao ametutaka tuwe waaminifu kwa Injili, kuiongokea Injili kwa kina, kuwa na fikra mpya na matazamo mpya wa mambo (Kifungu Na.15). Katika Waraka huo pia Baba ametuhimiza kuiheshimu Kweli zaidi ya chochote kile, kwa hoja kwamba Kweli ni Mungu (Kifungu 18) na kwamba kwa hoja hiyo hiyo, namna zetu za kuielezea imani yetu zisiwe kuzuizi katika mchakato wetu wa kutafuta Kweli (Kifungu Na:36).
Na tubarikiwe sote sawasawa na Efe.1:3.
LUKA ROKI MAGHALI CHAMAYOMBE
0787 765 759
0714 118 428
0753 298 707
Chamayombe37@gmail.com

0 comments:

Post a Comment